Swahili New Testament Bible

2nd Corinthians 13

Galatians

Return to Index

Chapter 1

1

 Mimi Paulo mtume, 

2

 na ndugu wote walio pamoja nami, tunayaandikia makanisa yaliyoko Galatia. Mimi nimepata kuwa mtume si kutokana na mamlaka ya binadamu, wala si kwa nguvu ya mtu, bali kwa uwezo wa Yesu Kristo na wa Mungu Baba aliyemfufua Yesu kutoka wafu. 

3

 Tunawatakieni neema na amani kutoka kwa Mungu Baba yetu na kutoka kwa Bwana Yesu Kristo. 

4

 Kristo alijitoa mwenyewe kwa ajili ya dhambi zetu kufuatana na mapenzi ya Mungu wetu na Baba, ili apate kutuokoa katika ulimwengu huu mbaya wa sasa. 

5

 Kwake yeye uwe utukufu milele! Amina. 

6

 Nashangaa kwamba muda mfupi tu umepita, nanyi mnamwasi yule aliyewaita kwa neema ya Kristo, mkafuata Habari Njema ya namna nyingine. 

7

 Lakini hakuna "Habari Njema" nyingine. Ukweli ni kwamba wako watu wanaowavurugeni, watu wanaotaka kuipotosha Habari Njema ya Kristo. 

8

 Lakini, hata kama mmoja wetu au malaika kutoka mbinguni, atawahubirieni Habari Njema tofauti na ile tuliyowahubirieni sisi, basi huyo na alaaniwe! 

9

 Tulikwisha sema, na sasa nasema tena: kama mtu yeyote anawahubirieni Habari Njema ya aina nyingine, tofauti na ile mliyokwisha pokea, huyo na alaaniwe! 

10

 Sasa nataka kibali cha nani: cha binadamu, ama cha Mungu? Au je, nataka kuwapendeza watu? Kama ningefanya hivyo, mimi singekuwa kamwe mtumishi wa Kristo. 

11

 Ndugu, napenda mfahamu kwamba ile Habari Njema niliyoihubiri si ujumbe wa kibinadamu. 

12

 Wala mimi sikuipokea kutoka kwa binadamu, wala sikufundishwa na mtu. Yesu Kristo mwenyewe ndiye aliyenifunulia. 

13

 Bila shaka mlikwisha sikia jinsi nilivyokuwa ninaishi zamani kwa kuzingatia dini ya Kiyahudi, na jinsi nilivyolitesa kanisa la Mungu kupita kiasi na kutaka kuliharibu kabisa. 

14

 Naam, mimi niliwashinda wengi wa wananchi wenzangu wa rika langu katika kuizingatia dini ya Kiyahudi, nikajitahidi sana kuyashika mapokeo ya wazee wetu. 

15

 Lakini Mungu, kwa neema yake, alikuwa ameniteua hata kabla sijazaliwa, akaniita nimtumikie. 

16

 Mara tu alipoamua kunifunulia Mwanae kusudi niihubiri Habari Njema yake kwa watu wa mataifa mengine, bila kutafuta maoni ya binadamu, 

17

 na bila kwenda kwanza Yerusalemu kwa wale waliopata kuwa mitume kabla yangu, nilikwenda kwanza Arabia, kisha nikarudi tena Damasko. 

18

 Ilikuwa tu baada ya miaka mitatu, ndipo nilipokwenda Yerusalemu kuonana na Kefa; nilikaa kwake siku kumi na tano. 

19

 Lakini sikuwaona mitume wengine isipokuwa Yakobo, ndugu yake Bwana. 

20

 Haya ninayowaandikieni, Mungu anajua; sisemi uongo. 

21

 Baadaye nilikwenda katika tarafa za Siria na Kilikia. 

22

 Wakati huo, mimi binafsi sikujulikana kwa jumuiya za Wakristo kule Yudea. 

23

 Walichokuwa wanajua ni kile tu walichosikia: "Mtu yule aliyekuwa akitutesa hapo awali, sasa anaihubiri imani ileile aliyokuwa anajaribu kuiangamiza." 

24

 Basi, wakamtukuza Mungu kwa sababu yangu. 

Galatians 2

 

 

 

Please Click the Ads.

Clicking the Ads helps us to keep this free Bible website open for everyone.

Thanks!

 

 

 

HTMLBible Software - Public Domain Software by johnhurt.com

 


Other Items are Available At These Sites: